Monday, October 19, 2015

MAMLAKA YA HALI YA HEWA TANZANIA (TMA) WASISITIZA KUWEPO KWA El-Nino

MAMLAKA ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imeendelea kuwatahadharisha wananchi kuwa mvua kubwa za el-Nino zinatarajiwa kunyesha kuanzia wiki ya mwisho ya Septemba, mwaka huu na mwanzoni mwa mwezi Oktoba kama ilivyokuwa imetabiriwa kutokana na mifumo ya hali ya hewa kuzidi kuonesha hali hiyo.

Imeeleza kuwa mvua ndogo ndogo zinazoendelea kunyesha maeneo mbalimbali nchini, ikiwemo jiji la Dar es Salaam si mvua hizo za msimu wa vuli yaani Oktoba hadi Desemba mwaka huu, ila ni mabadiliko ya hali ya hewa katika eneo la bahari.
Mkurugenzi wa TMA, Dk Agness Kijazi alisema hayo jana wakati akitoa mrejeo wa mwenendo wa mifumo ya hali ya hewa.

Alisema mvua za el-Nino bado zipo na kutoa msisitizo kuwa inatarajia kwa kiasi kikubwa kuchangia mwenendo wa mvua nchini katika kipindi hicho, kwani hali ya joto mashariki mwa bahari ya Pasifiki inaonesha kuwepo kwa hali ya el-Nino.

Alisema joto lipo zaidi ya nyuzi joto 2.5 juu ya wastani na linatarajia kuendelea kuongezeka kufikia nyuzi joto 3.0 kuelekea mwezi Novemba mwaka huu.

Dk Kijazi alisema pia magharibi mwa bahari ya Hindi hali ya joto ipo juu ya wastani na inatarajiwa kuendelea kuwa juu ya wastani kiasi cha nyuzi joto zaidi ya 2.0 kufikia mwezi Novemba mwaka huu wakati mashariki mwa bahari, joto zaidi chini ya wastani kufikia nyuzi joto -1.5.

“Pamoja na viashiria vingine vya hali ya hewa vinatarajia kusababisha mvua nyingi hususan katika maeneo mengi ya kaskazini mwa nchi ambayo hupata misimu miwili ya mvua kwa mwaka,” alisema.
Hivyo alitaka mamlaka zinazohusika kuchukua tahadhari zinazotakiwa ili kukabiliana na madhara yanayoweza kutokea kutokana na mvua hizo kubwa zinazotarajia kuanza kunyesha hivi karibuni.

0 comments:

Post a Comment

 
Design by Free WordPress Themes | Bloggerized by Lasantha - Premium Blogger Themes | Best WordPress Themes